Na Dotto Kwilasa,DODOMA
MKURUGENZI wa Mafunzo ya Ufundi Stadi -VETA,Abdallah Ngodu amesema kuwa maonesho ya wiki ya Ubunifu kwa mwaka huu yamekuwa tofauti kwani wamepewa nafasi ya kuwa na siku maalumu kwa ajili ya VETA ambayo imekwenda kwa jina la “VETA DAY”
Amesema kupitia wiki hiyo wameweza kuandaa vitu mbalimbali kwajili ya maonesho ya bunifu zao lakini pia wamekuwa na matukio muhimu ikiwemo mdahalo kwa ajili ya umuhimu wa elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi- katika ubunifu.
Amesema hayo Jijini Dodoma kwenye maonesho yanayoendelea ikiwa ni wiki ya ubunifu ambayo inawakutanisha wabunifu mbalimbali kutoka ndani na nje ya Nchi ambayo ilianza Aprili 24,2023 katika uwanja wa Jamhuri na yanatarajia kumalizika Ijumaa Aprili 28 mwaka huu yaliyoandaliwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
“Mdahalo huo utasimamiwa na Msemaji Mkuu wa Serikali ndugu Gerson Msigwa katika (Clubhouse),pia tunamashindano ya umahiri wa vijana ambao wanapata mafunzo katika vyuo vyetu,"alisema.
Alisema lengo la mashindano hayo ni kujua vijana wamepata ujuzi na wameweza kumudu stadi zipi.
“Bahati nzuri katika hawa vijana waliomaliza vyuo vyetu wapo ambao wamemaliza vyuo vikuu lakini kutokana na mazingira magumu ya ajira basi wamekuja VETA na wameweza kutengeneza vitu mbalimbali,”alisema.
Naye Mkurugenzi wa Idara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu Prof.Maulilio Kipanyula alisema kuwa Maonesho ya wiki ya Ubunifu mwaka 2023 yamekuwa tofauti kwani imeanzi katika ngazi za mikoa na huko wabunifu walianza kuonesha bunifu zao katika ngazi hizo na sasa maonesho hayo yamefikia katika ngazi ya taifa hivyo imewapa nafasi wabunifu wengi kuonesha bunifu zao.
Prof. Kipanyula aliongeza kuwa katika maonesho hayo kutakuwa na siku maalumu kwa ajili ya Taasisi za VETA na Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC)
“VETA leo wameonesha bunifu zao na ndio maana leo ni VETA DAY dhumuni ni kuona ni namna gani uwekezaji uliofanywa na Serikali ya awamu ya sita katika elimu ya ufundi imefanyiwa kazi na kuzalisha wabunifu wenye uwezo wa kuigiza sokoni bunifu kwa ajili ya kutatua changamoto za jamii,”alisema
Kwa upande wake wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule amewapongeza Mamlaka ya Elimu na mafunzo ya ufundi stadi(VETA)kwa mafunzo mazuri wanayotoa kwa vijana hadi kupelekea kuwa wabunifu.
“Tunafahamu kwamba Serikali imekuwa ikihangaika muda mrefu jinsi gani ya kuzuia ajali sasa kijana wa kitanzania ametupatia ufumbuzi tunaimani teknolojia hiyo itaendelea kitumika kupunguza ajali nchini,
"Nimeona na kusikia ile miwazi inavyofanyakazi na jinsi inavyomkumbusha dereva kuwa anasinzia kiukweli ubunifu huu ni wa kipekee kwani utasaidia sana hasa kwenye suala la usalama barabarani,"alisema Senyamule.
“Nimetembelea mabanda mengi nimeona mabadiliko makubwa ya matumizi ya teknolojia na ubunifu mkubwa,nipongeze sana Wizara ya Elimu kwa kazi nzuri wanayofanya katika kuandaa yote haya,”alisema.
